Ugonjwa Wa Kaswende – Syphilis . Ni Nini Chanzo Na Tiba Yake?

Kaswende - hatua ya pili ya kaswende

 

Kaswende ni ugonjwa unaoambukiza haraka sana, mara nyingi kupitia ngono. Ugonjwa huu huenezwa kwa kugusa moja kwa moja mchubuko wa kaswende (syphilitic sore) uliopo kwenye ngozi, au kwenye ngozi laini zenye majimaji za ukeni, kwenye mkundu, na midomo. Kwa hiyo njia kuu ni kupitia ngono ya kawaida, ya kutumia midomo na ile ya kinyume na maumbile. Mara chache ugonjwa huu huweza kuambukiza kwa kubusiana au kugusana miili. Pamoja na kuwa ugonjwa huambukiza kupitia michubuko, mara nyingi michubuko hatarishi haitambulikani. Mtu aliyeambukizwa huwa hajielewi na hivyo kumwambukiza mpenzi wake.

Kaswende haiambukizi kwa kuchangia vyoo, vitasa vya milango, mabwawa ya kuogelea, kuchangia nguo au vyombo vya chakula.

 

Chanzo Cha Kaswende Ni Nini?

 

Kaswende husababishwa na bakteria aitwaye Treponema pallidum, ambaye pia huitwa spirochetes kutokana na umbo lake la mzunguko. Viumbe hawa hujipenyeza kwenye ngozi laini inayotanda kwenye midomo au sehemu nyeti.

Mwanamke mwenye mimba na ana ugonjwa huu anaweza kumwambukiza mtoto aliye tumboni kupitia placenta au wakati wa kuzaliwa. Aina hii ya kaswende huitwa congenital syphilis, na inaweza kusababisha kujifungua mtoto mfu au mtoto akafa muda mfupi baada ya kuzaliwa. Watoto wengi hawaonyeshi dalili wanapozaliwa. Baadaye watoto huota vijipele, hupata matatizo ya meno, na kubonyea kwa mfupa wa pua – hali inayoitwa saddle nose, kuwa viziwi, kuwa na watoto wa jicho na kifafa.

 

Dalili Za Kaswende

 

Kuna hatua nne za ugonjwa huu wa kaswende. Ni dalili gani utaziona, inategemeanan na ugonjwa upo katika hatua ipi katika hizi nne. Hatua hizi zinaweza kuingiliana na dalili si lazima zitokee kwa mtiririko ule ule. Unaweza pia ikawa na kaswende na usione dalili zo zote kwa miaka kadhaa.

Lakini, hata kama hujaona dalili zo zote, bado unaweza kumwambukiza mpenzi wako.

 

Hatua Ya kwanza Ya Kaswende – Primary Syphilis

 

Dalili za hatua ya kwanza huonekana siku 10 hadi miezi 3 baada ya kuambukizwa. Unaweza pia kuona mitoki maeneo ya kinena chako.

Mara nyingi, dalili ya kwanza kabisa imayoonekana ni aina ya mchubuko mdogo, mgumu  usio na maumivu (chancre) juu ya ngozi (unaweza ukatokewa na michubuko zaidi ya mmoja). Mchubuko huu aghalabu hutokea pahala ambapo bakteria waliingilia. Ni mchubuko usio na maumivu, na unaweza kutokea sehemu ya uficho kama kwenye uke au ndani ya rektamu. Unaweza usijue kama una mchubuko huu.

Mchubuko huu utapona wenyewe katika wiki 3 hadi 6. Haimaanishi kuwa umepona. Maana yake ni kwamba unaingia hatua ya pili ya ugonjwa wa kaswende.

 

 

 

 

Kaswende - mchubuko wa kaswende

 

 

Kaswende - mchubuko wa kaswende kwenye uke

 

Hatua Ya Pili Ya Kaswende – Secondary Syphilis

Wiki 2 hadi 10 baada ya mchubuko wa kwanza kutokea, unaweza kuona dalili zifuatazo:

. Vipele vidogo mwilini, vya mviringo vyenge rangi ya nyekundu au vyenye wekundu wa kahawia. vijipele huota mara nyingi vikianzia mgongoni na kuenea mwili mzima, pamoja na kwenye viganja vya mikono na kwenye nyayo.

. Michubuko inayofanana na chunjua huotokea mdomoni, ukeni au kwenye mkundu
. Homa
. Kuvimba tezi
. Kukonda
. Kupunyuka nywele
. Kuumwa kichwa
. Uchovu mkali
. Maumivu ya misuli

Tiba sahihi isipotolewa, ugonjwa utatoweka tena na kurudi tena baadaye, mara nyingi baada ya mwaka mmoja. Hata kama dalili hazionekani, ugonjwa bado upo na unazidi kuwa mbaya zaidi, na unaweza kumwambukiza mwenzi wako.

 

Kaswende - vipele vya kaswende

 

Michubuko inayofanana na chunjua hutokea kwenye sehemu za midomo na mkundu. Vile vile kutatokea maumivu ya misuli, homa, kukauka koo, kuvimba tezi, kupunyuka nywele, kukonda na uchovu wa mwili.

Latent Syphilis

Kama tiba ya kaswende ya hatua ya pili haitatolewa, ugonjwa utaendelea kwenye hatua iitwayo latent stage. Katika hatua hii inayoweza kudumu kwa miaka kadhaa, mwili utautunza ugonjwa bila kuonyesha dalili zo zote. Pamoja na kuwa hakuna dalili zo zote zitakazoonekana, ugonjwa huu unaweza kuendelea kwenye hatua ya mwisho.

 

Hatua Ya Tatu Ya Kaswende – Tertiary syphilis

Asilimia 15 ya watu ambao hawakupata tiba kwenye hatua ya pili ya kaswende watapata kaswende ya hatua ya tatu – tertiary syphilis.

Hii ni hatua ya mwisho, na mbaya zaidi ya zote. Hatua hii hutokea miaka 10 hadi 30 baada ya maambukizi ya awali. Unaweza kupata ulemavu wa kudumu wa kiungo cha mwili au kifo. Madhara yanaweza kuwa:

. Matatizo ya kwenye ubongo
. Kiharusi
. Maambukizi kwenye ngozi laini inayouzunguka ubongo au uti wa mgongo
. Ganzi
. Ukiziwi
. Kutoona vizuri au upofu
. Usahaulifu (dementia)
. Matatizo ya valvu za moyo
. Aneurysm
. Magonjwa ya mishipa ya damu

 

Tiba Ya Kaswende

 

Kuwahi kumpa tiba mgonjwa wa kaswende ni muhimu kwani kuchelewa kunaweza kumletea madhara makubwa ya mwili au kifo. Kama ugonjwa haujazidi mwaka mmoja, mara nyingi dozi moja ya ya penicillin hutosha. Kwa wale wanaopata madhara kwa kutumia penicillin, tetracycline, doxycycline, au antibiotic yo yote inaweza kutumika.

Kaswende iliyoendelea kwenye hatua nyingine, dozi nyingine zitahitajika.

Katika kurasa nyingine tumejadili  ugonjwa wa kisonono (Gonorrhoea) na ugonjwa wa UKIMWI.

Ndugu msomaji, uwe huru kuuliza maswali au kutoa maono yako kuhusu mada yetu ya leo. Tunaahidi kukujibu kwa wakati mwafaka.

 

Kwa mawasiliano tuma ujumbe wako kupitia ukurasa huu kwa kujaza fomu hapa chini , au tuma barua pepe kwa anuani promota927@gmail.com au piga simu kwenye nambari zifuatazo: 0655 858027 au 0756 181651.

 

Tafadhali ungana nasi kwenye ukurasa wa facebook wa LINDA AFYA YAKO ili upate mfululizo wa mada zetu zinazohusu afya ya binadamu na jinsi ya kuanza na kufanya biashara za mtandao zinazohusu virutubisho vya mwili kwa mtaji mdogo kabisa. Tunaomba uweke LIKE kwenye ukurasa huo endapo utakuwa umependezewa na mada zetu.